![](https://isaackzake.co.tz/wp-content/uploads/2021/10/called-by-God.jpg)
Utangulizi
Karibu sana ndugu yangu msomaji ni siku nyingine tena tumepewa na Mungu kwa ajili ya kuendelea kujifunza zaidi misingi ya chakula cha kiroho ili kutuwezesha kufanya mapenzi yake na kumtumikia kwa furaha na upendo siku ya leo.
‘Akasema kwa sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu’ Yn.6:65
Mambo ya kujifunza
- Maisha yetu siku zote na hatma yetu ipo ndani ya kusudi lake Mungu. Asili yetu sisi ni Mungu mwenyewe na kwa upendo wake anaturejesha kwake
- Katika huduma yake Bwana Yesu alikutana na aina mbalimbali ya watu ambao walimfuata na kusikiliza mafundisho yake. Lakini si wote walikubali kuambatana naye katika yale aliyofundisha.
- Mungu kwa neema yake ametufunulia sisi wanadamu wote jinsi ya kuufikia wokovu wa maisha yetu kupitia Mwana wake Yesu Kristo. Maandiko yanaeleza wazi jinsi Mungu alivyoupenda ulimwengu kiasi cha kumtoa mwanawe wa pekee kwa ajili yetu sote.
- Kiwango cha upendo wa Mungu kwetu kilimsukuma Yeye kushuka na kuikamilisha kazi ya msalaba kwa kila atakayemwamini aweze kupata msamaha na ondoleo la dhambi. Hii ni fursa ya kila mwanadamu.
- Sisi sote kila mmoja wetu anao wajibu wa pekee kuitikia wito huu wa Mungu ambao aliutoa zaidi ya miaka 2000 tangu Bwana Yesu kusulubiwa kwa ajili ya ulimwengu wote.
- Mungu halazimishi mtu yeyote kumfuata Yesu lakini tunapata neema hiyo kwa kusikiliza neno lake na kuwa na itikio la imani katika kile anachotueleza.
- Leo kama utaisikia sauti ya Baba aliye asili yako na yangu basi chukua hatua ya kumwendea Yesu Kristo kwani ndiye pekee aliyewekwa kuwa mpatanishi baina ya Mungu na wanadamu wote.
MAOMBI LEO
Ndugu yangu ikiwa ndani yako unashuhudiwa bado huna uhakika wa maisha yako na kumjua Mungu ipasavyo, ujue unahitaji ufahamu huo kupitia uzima wa Mungu kuingia ndani yako. Karibu ufuatane nami katika kuomba maombi haya ili uzima wa Mungu ukae ndani yako sasa;
‘Ee Mungu Baba ninakushukuru kwa neno lako la uzima, asante kwa sadaka ya Mwana wako Yesu Kristo pale msalabani kwa ajili yangu. Bwana Yesu ninakiri udhaifu wangu na wasi wasi wangu wa kupotea milele endapo nitaondoka katika maisha haya. Ninaomba unisamehe dhambi zangu zote nilizofanya na hata kuondoa asili ya dhambi ndani yangu, unitakase kwa Damu yako takatifu. Ninaomba ufute jina langu katika kitabu cha hukumu na kuliandika katika kitabu cha uzima. Ninaomba uniokoe na kunifanya upya ndani yangu kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Uingie ndani yangu na kuniongoza tangu sasa na hata milele’ Amen.
Ikiwa umefanya sala hii kwa imani, Mungu kwa neema yake amekurehemu na kukusamehe kabisa, hata kama umefanya dhambi yeye ameisafisha na kuisahau. Unapaswa na wewe kujisamehe na kumfuata Yesu tangu sasa.
Mungu mwenyewe aliyetuita ni mwaminifu, naye atafanya katika Jina la Mwana wake Mpendwa Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wa maisha yetu. Amen
‘Utupe leo riziki yetu’
Isaack Zake
Wakili, Mwalimu na Mshauri
Wasiliana na Isaack Zake kwa barua pepe info@isaackzake.co.tz au kwa simu 0713 888 040 kwa ushauri na mafundisho. Mungu akubariki sana
Leave a Reply
Want to join the discussion?Feel free to contribute!