Utangulizi
Karibu sana ndugu yangu msomaji ni siku nyingine tena tumepewa na Mungu kwa ajili ya kuendelea kujifunza zaidi misingi ya chakula cha kiroho ili kutuwezesha kufanya mapenzi yake na kumtumikia kwa furaha na upendo siku ya leo.
‘Hiki ni chakula kishikacho kutoka mbinguni; kwamba akile wala asife’ Yn.6:50
Mambo ya kujifunza
- Bwana Yesu anasema kipo chakula ambacho mtu anaweza kula lakini asife. Katika somo lililopita tuliona ya kuwa unaweza kula chakula lakini ukafa. Leo anatueleza aina ya chakula ambacho mtu akila hatokufa.
- Kila mmoja wetu anatamani sana kuishi daima na si tu kuishi muda mrefu. Pamoja na umri tunaokuwa nao lakini bado tusingetaka kufa. Linapotajwa swala la kifo hakuna ambaye ana ujasiri wa kusimama na tayari kila mmoja wetu anajua ya kuwa siku moja atakufa na kuondoka katika maisha haya.
- Lakini maneno ya Yesu anatueleza ya kuwa kipo aina ya chakula ambacho mtu akila hatokufa na hiki ni chakula kishukacho kutoka mbinguni. Tulijifunza habari ya maisha na kifo ya kuwa maisha ni muunganiko wa uhusiano wako na Mungu na kifo ni utengano baina ya maisha yako binafsi na Mungu.
- Suala la kifo au kutengena baina yako na Mungu ni kubwa sana kuliko kifo cha kutenganishwa mwili na roho yako. Watu wengi wanaogopa kifo cha kimwili kuliko kifo cha kiroho. Kifo cha mwili ni cha muda tu lakini kifo cha kiroho ni cha milele.
- Ingawa tunafahamu juu ya uwepo wa kifo cha kimwili kwa ajili ya kila mwanadamu aliyezaliwa hatupaswi kukiogopa kwani ni kitu cha sekunde chache sana na tayari mtu anaingia katika mfumo wa maisha mengine ya kuwa na Mungu milele au kutengwa na Mungu milele.
- Chakula kishukacho kutoka mbinguni sasa kwa ajili yetu ndicho kinaweza kutuvusha katika wakati huu na kutusaidia kuishi badala ya kufa. Unahitaji maisha ya milele au unahitaji kuishi siku zote bila mauti au kifo kukuathiri? Basi kula chakula kishukacho kutoka mbinguni.
MAOMBI LEO
Ndugu yangu ikiwa ndani yako unashuhudiwa bado huna uhakika wa maisha yako na kumjua Mungu ipasavyo, ujue unahitaji ufahamu huo kupitia uzima wa Mungu kuingia ndani yako. Karibu ufuatane nami katika kuomba maombi haya ili uzima wa Mungu ukae ndani yako sasa;
‘Ee Mungu Baba ninakushukuru kwa neno lako la uzima, asante kwa sadaka ya Mwana wako Yesu Kristo pale msalabani kwa ajili yangu. Bwana Yesu ninakiri udhaifu wangu na wasi wasi wangu wa kupotea milele endapo nitaondoka katika maisha haya. Ninaomba unisamehe dhambi zangu zote nilizofanya na hata kuondoa asili ya dhambi ndani yangu, unitakase kwa Damu yako takatifu. Ninaomba ufute jina langu katika kitabu cha hukumu na kuliandika katika kitabu cha uzima. Ninaomba uniokoe na kunifanya upya ndani yangu kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Uingie ndani yangu na kuniongoza tangu sasa na hata milele’ Amen.
Ikiwa umefanya sala hii kwa imani, Mungu kwa neema yake amekurehemu na kukusamehe kabisa, hata kama umefanya dhambi yeye ameisafisha na kuisahau. Unapaswa na wewe kujisamehe na kumfuata Yesu tangu sasa.
Mungu mwenyewe aliyetuita ni mwaminifu, naye atafanya katika Jina la Mwana wake Mpendwa Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wa maisha yetu. Amen
‘Utupe leo riziki yetu’
Isaack Zake
Wakili, Mwalimu na Mshauri
Wasiliana na Isaack Zake kwa barua pepe info@isaackzake.co.tz au kwa simu 0713 888 040 kwa ushauri na mafundisho. Mungu akubariki sana
Leave a Reply
Want to join the discussion?Feel free to contribute!