Utangulizi
Karibu sana ndugu yangu msomaji ni siku nyingine tena tumepewa na Mungu kwa ajili ya kuendelea kujifunza zaidi misingi ya chakula cha kiroho ili kutuwezesha kufanya mapenzi yake na kumtumikia kwa furaha na upendo siku ya leo.
‘Mimi ndimi chakula cha uzima’ Yn.6:48
Mambo ya kujifunza
- Tumeona juu ya kumfahamu Yesu kama chakula cha Uzima katika andiko lililonukuliwa hapo juu. Lakini haitoshi tu sisi kufahamu Yesu kama chakula bali ina maana gani sisi waamini na ni hatua gani tunapaswa kuzichukua kila siku?
- Kama tulivyo na mipango ya kupata chakula cha kimwili kila siku, ndivyo Mungu anavyotutazamia tuwe na mipango hiyo hiyo kwa ajili ya kupata chakula cha kiroho kila siku ili kuendeleza maisha yetu ya kila siku. Mungu wetu ana kiu kubwa kwetu sisi tumtazame Yesu Kristo kama chakula cha uzima kuliko tunavyotazama chakula cha miili yetu. Hii ni kwa sababu ya umuhimu na faida kubwa tunayoipata katika kula chakula kitokacho kwa Mungu.
- Bila kufahamu kile kinachofanywa na chakula cha uzima ambacho ni Yesu Kristo ndani yetu hatuwezi kukitafuta wala kuwa na mpango nacho katika chakula cha siku ya leo. Watu wengi wanaomjia Yesu wanakubali kuokolewa kwa dhabihu yake pale msalabani hawaendi zaidi ya hapo. Haitoshi tu kuokoka kwani hapo ni kama umefunguliwa mlango wa nyumba, lakini unahitaji kuingia ndani zaidi.
- Neno la Yesu katika maisha ya mtu kila siku lina umuhimu mkubwa sana wa kuboresha maisha na mahusiano baina ya mtu husika na Yesu Kristo. Ndio maana Yesu anasema Yeye ndiye chakula cha uzima. Tunamuhitaji Yesu pekee na maisha yetu yatakuwa salama. Si kwa ajili ya maisha baada ya kifo bali wakati huu tulipo duniani katika safari yetu tunahitaji ‘kumla Yesu’ au kulisikia neno lake kama chakula cha uzima.
- Yapo maneno mengi sana katika madhabahu nyingi sana, nyingine ni za dini ya Kikristo na nyingine kutoka imani kadhaa wa kadha. Kelele zipo nyingi sana duniani kila leo. Lakini kama unahitaji uzima yaani uhai wa roho yako na nafsi yako na kisha uwezo wa kuzitenda kazi za Mungu unamuhitaji Yesu Kristo na neno lake kwa ajili yako.
- Si kila neno linalotoka kwenye biblia ni kwa ajili yako. Watu wengi wanahangaishwa na maneno yanayotoka kwenye madhabahu na wanatetemeshwa na maagizo ya wanadamu wakidhani yanatoka kwa Mungu. Ndio maana unamuhitaji Yesu mwenyewe aseme na wewe binafsi.

- Kama unamwamini Yesu Kristo lakini hupati hamu ya chakula cha kiroho au kusikia neno la Kristo basi kuna shida mahali katika aina ya mafundisho unayopokea siku kwa siku. Tunapaswa kupata neno la Kristo kwa ajili yetu kila siku ili kuhuisha mahusiano yako na Kristo na kuingia kazini.
MAOMBI LEO
Ndugu yangu ikiwa ndani yako unashuhudiwa bado huna uhakika wa maisha yako na kumjua Mungu ipasavyo, ujue unahitaji ufahamu huo kupitia uzima wa Mungu kuingia ndani yako. Karibu ufuatane nami katika kuomba maombi haya ili uzima wa Mungu ukae ndani yako sasa;
‘Ee Mungu Baba ninakushukuru kwa neno lako la uzima, asante kwa sadaka ya Mwana wako Yesu Kristo pale msalabani kwa ajili yangu. Bwana Yesu ninakiri udhaifu wangu na wasi wasi wangu wa kupotea milele endapo nitaondoka katika maisha haya. Ninaomba unisamehe dhambi zangu zote nilizofanya na hata kuondoa asili ya dhambi ndani yangu, unitakase kwa Damu yako takatifu. Ninaomba ufute jina langu katika kitabu cha hukumu na kuliandika katika kitabu cha uzima. Ninaomba uniokoe na kunifanya upya ndani yangu kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Uingie ndani yangu na kuniongoza tangu sasa na hata milele’ Amen.
Ikiwa umefanya sala hii kwa imani, Mungu kwa neema yake amekurehemu na kukusamehe kabisa, hata kama umefanya dhambi yeye ameisafisha na kuisahau. Unapaswa na wewe kujisamehe na kumfuata Yesu tangu sasa.
Mungu mwenyewe aliyetuita ni mwaminifu, naye atafanya katika Jina la Mwana wake Mpendwa Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wa maisha yetu. Amen
‘Utupe leo riziki yetu’
Isaack Zake
Wakili, Mwalimu na Mshauri
Wasiliana na Isaack Zake kwa barua pepe info@isaackzake.co.tz au kwa simu 0713 888 040 kwa ushauri na mafundisho. Mungu akubariki sana.
Leave a Reply
Want to join the discussion?Feel free to contribute!