
Utangulizi
Karibu sana ndugu yangu msomaji ni siku nyingine tena tumepewa na Mungu kwa ajili ya kuendelea kujifunza zaidi misingi ya chakula cha kiroho ili kutuwezesha kufanya mapenzi yake na kumtumikia kwa furaha na upendo siku ya leo.
‘Amin, amin, nawaambia, Yeye aaminiye yuna uzima wa milele’ Yn.6:47
Mambo ya kujifunza
- Maandiko haya yanatuonesha maneno ya Yesu Kristo mwenyewe akizungumzia suala la wale watakao amini maneno yake ya kuwa wana uzima wa milele. Je, ana maana gani anaposema ‘yuna uzima wa milele’?
- Ili kufahamu zaidi kuhusu uzima wa milele ni muhimu kurejea kile kilichotokea pale Eden wakati wazazi wetu wa asili walipoasi kwa kwenda kinyume cha agizo la Mungu. Adhabu ya mauti ilitamkwa dhidi yao mara tu walipoasi. Lakini tunaona ya kuwa pamoja na kuambiwa hakika watakufa tunaona waliishi miaka mingi sana. Adam aliishi zaidi ya miaka 900.
- Hii ina maana kifo ni zaidi ya kutenganishwa mwili na roho ya mwanadamu. Maana halisi ya kifo ni kutenganishwa na Mungu au kukosa uhusiano sahihi na Mungu. Kitendo cha kwenda kinyume na agizo la Mungu pale Eden wakati huo huo kifo kilitokea katika maisha ya mwanadamu na hivyo kutengwa na Mungu.
- Sasa Bwana Yesu anapozungumzia suala la aaminiye yuna uzima wa milele ana maana pana zaidi ya maisha baada ya kifo cha kimwili. Ni kweli kama mtu ana mahusiano na Mungu anayo nafasi ya kuishi milele katika uwepo wa Mungu. Hali kadhalika yule asiye na mahusiano sahihi na Mungu pia huishi milele lakini nje ya uwepo wa Mungu. Hii ni kwa sababu roho ya mwanadamu haifi au kupotea kabisa itaishi na Mungu au katika adhabu milele.
- Kwa maana nyingine Bwana Yesu anatueleza juu ya uzima wa milele si kwamba tunaupata baada ya kuondoka katika maisha haya, bali tunaupata pindi tu tunapomwamini. Kama vile mauti tuliipata pindi tulipoasi pale Eden na kila mmoja aliyezaliwa na mwanadamu anarithi hali ya mauti vivyo hivyo uzima wa milele tunaupata pindi tu tunapokubali na kumwamini Yesu Kristo kama Adam II.
- Uzima wa milele ndani ya mtu ndio mbegu ya Mungu ya kumwezesha mwanadamu kumjua Mungu na Yesu Kristo katika maisha haya ya sasa na hata baada ya kuondoka katika mwili. hivyo ni wito wa Bwana Yesu kwetu sisi sote kumwamini SASA ili kuupata UZIMA WA MILELE SASA na kuendelea nao hata baada ya kuzikwa kwa mwili huu wenye asili ya dunia.
- Hakuna mwanadamu anayeweza kumjua Mungu sawasawa na Yesu Kristo aliyetumwa kwa ajili yetu bila kuwa na uzima wa Mungu ndani yake. Harakati zote tunazoziona za dini zote hapa duniani hata dini ya Kikristo kama hazimsaidii mtu kuupokea uzima wa Mungu ndani yake hazina maana katika kuleta mabadiliko ya kweli kimaisha. Ndio maana Yesu Kristo hakuanzisha dini bali alikuja kurejesha mahusiano yaliyopotea baina ya Mungu na wanadamu.
- Yesu Kristo alikuja kama Adam II ili kuwarudisha wanadamu wote katika uhusiano sahihi na Mungu wao bila kujali dini zao, makabila yao, rangi zao, asili zao, koo zao au mataifa yao. Wote tunapokea neema ile ile ndani ya Kristo ya kurudishwa katika uhusiano sahihi na Mungu kupitia uzima wa milele sasa.
MAOMBI LEO
Ndugu yangu ikiwa ndani yako unashuhudiwa bado huna uhakika wa maisha yako na kumjua Mungu ipasavyo, ujue unahitaji ufahamu huo kupitia uzima wa Mungu kuingia ndani yako. Karibu ufuatane nami katika kuomba maombi haya ili uzima wa Mungu ukae ndani yako sasa;
‘Ee Mungu Baba ninakushukuru kwa neno lako la uzima, asante kwa sadaka ya Mwana wako Yesu Kristo pale msalabani kwa ajili yangu. Bwana Yesu ninakiri udhaifu wangu na wasi wasi wangu wa kupotea milele endapo nitaondoka katika maisha haya. Ninaomba unisamehe dhambi zangu zote nilizofanya na hata kuondoa asili ya dhambi ndani yangu, unitakase kwa Damu yako takatifu. Ninaomba ufute jina langu katika kitabu cha hukumu na kuliandika katika kitabu cha uzima. Ninaomba uniokoe na kunifanya upya ndani yangu kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Uingie ndani yangu na kuniongoza tangu sasa na hata milele’ Amen.
Ikiwa umefanya sala hii kwa imani, Mungu kwa neema yake amekurehemu na kukusamehe kabisa, hata kama umefanya dhambi yeye ameisafisha na kuisahau. Unapaswa na wewe kujisamehe na kumfuata Yesu tangu sasa.
Mungu mwenyewe aliyetuita ni mwaminifu, naye atafanya katika Jina la Mwana wake Mpendwa Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wa maisha yetu. Amen
‘Utupe leo riziki yetu’
Isaack Zake
Wakili, Mwalimu na Mshauri
Wasiliana na Isaack Zake kwa barua pepe info@isaackzake.co.tz au kwa simu 0713 888 040 kwa ushauri na mafundisho. Mungu akubariki sana.
Leave a Reply
Want to join the discussion?Feel free to contribute!