
Utangulizi
Karibu sana ndugu yangu msomaji ni siku nyingine tena tumepewa na Mungu kwa ajili ya kuendelea kujifunza zaidi misingi ya chakula cha kiroho ili kutuwezesha kufanya mapenzi yake na kumtumikia kwa furaha na upendo siku ya leo.
‘Amin, amin, nawaambia, Yeye aaminiye yuna uzima wa milele’ Yn.6:47
Mambo ya kujifunza
- Suala la kumfuata Yesu Kristo ni imani juu ya kile anachosema. Maisha ya mwanadamu yeyote yanategemea kile anachoamini. Kila mtu ndani yake anaishi kwa imani. Imani ni mfumo wa maisha ya kila mwanadamu, kwa maana nyingine hakuna mwanadamu asiye na imani bila kujali anachoamini.
- Tofauti zetu wanadamu hazipo kwenye mfumo wa imani bali aina za imani au vyanzo vya taarifa tunazoziamini. Kila mmoja ana imani lakini tofauti yetu ni aina za imani tunazoamini chanzo chake ni nini.
- Huu ndio msingi wa uwepo wa dini nyingi sana duniani na madhehebu kadhaa. Nadhani unafahamu juu ya dini ya kikisto ya kuwa wote tunamwamini Yesu Kristo lakini mbona madhehebu ni mengi sana wakati Yesu Kristo ni mmoja? Hii ina maana wapo viongozi wengi wanaoongoza watu kwa Kristo kulingana na misingi ya namna walivyoamini. Hili ni eneo moja tu la dini ambalo tumeangalia achilia mbali madhehebu mengine katika dini nyingine.
- Lakini msingi wa neno hili analosema Yesu ‘yeye aaminiye yuna uzima wa milele’ hapa si kila anayeamini kile anachoamini bali kile anachosema Yesu Kristo. Si kila imani inaweza kumwakikishia mwanadamu uzima wa milele bali Yesu peke yake ndiye mwenye uwezo huo.
- Ndio maana hupaswi mtu kubishana kuhusiana na imani ya mtu mwengine kwani kila mmoja ana imani yake, wala hupaswi kushindanisha imani yako na ya mtu mwengine bali fundisha kile unachoamini ili yumkini mtu akipima anaweza kufanya uchaguzi sahihi kwa ajili yake binafsi.
- Suala la uzima wa milele analozungumza Yesu Kristo katika maneno haya ni suala binafsi wala hakuzungumza kijumla au na kundi la wakristo bali alisema na kila mtu anayetaka kuamini maneno yake ya kwamba atapata uzima wa milele, ndio maana alisisitiza aliposema ‘amin, amin…’ ina maana ya kweli wala haiwezi kubadilika kile anachosema ndivyo kilivyo ukitaka kuamini basi inakuwa kwako kama ulivyoamini.
- Unaweza ukawa umezaliwa katika familia au ukoo au dhehebu au dini fulani ambayo msingi wa imani yake haujajengwa kwa Yesu Kristo bali kwa watu au watume wengine lakini ukichunguza juu ya imani yako unaweza kuona kuna maneno yana mashaka, usiogope Yesu anasema yeye aaminiye maneno yake yuna uzima wa milele. Hapa si suala la dini au familia hili ni suala binafsi baina ya mtu na Mungu.
MAOMBI LEO
Ikiwa ndani yako ungependa kuona ahadi ya Bwana Yesu inatimia ya kuwa usipotee milele bali upate kufufuliwa siku ya mwisho na kwamba unaona uhusiano wako kwa sasa na Bwana Yesu si sahihi na unashuhudiwa moyoni ya kuwa endapo leo ni siku yako ya mwisho kuna uwezekano wa hukumu, basi chukua hatua na kubadili mkondo wa historia yako kwa kusali pamoja name
‘Ee Mungu Baba ninakushukuru kwa neno lako la uzima, asante kwa sadaka ya Mwana wako Yesu Kristo pale msalabani kwa ajili yangu. Bwana Yesu ninakiri udhaifu wangu na wasi wasi wangu wa kupotea milele endapo nitaondoka katika maisha haya. Ninaomba unisamehe dhambi zangu zote nilizofanya na hata kuondoa asili ya dhambi ndani yangu, unitakase kwa Damu yako takatifu. Ninaomba ufute jina langu katika kitabu cha hukumu na kuliandika katika kitabu cha uzima. Ninaomba uniokoe na kunifanya upya ndani yangu kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Uingie ndani yangu na kuniongoza tangu sasa na hata milele’ Amen.
Ikiwa umefanya sala hii kwa imani, Mungu kwa neema yake amekurehemu na kukusamehe kabisa, hata kama umefanya dhambi yeye ameisafisha na kuisahau. Unapaswa na wewe kujisamehe na kumfuata Yesu tangu sasa.
Mungu mwenyewe aliyetuita ni mwaminifu, naye atafanya katika Jina la Mwana wake Mpendwa Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wa maisha yetu. Amen
‘Utupe leo riziki yetu’
Isaack Zake
Wakili, Mwalimu na Mshauri
Wasiliana na Isaack Zake kwa barua pepe info@isaackzake.co.tz au kwa simu 0713 888 040 kwa ushauri na mafundisho. Mungu akubariki sana.
Leave a Reply
Want to join the discussion?Feel free to contribute!