
Utangulizi
Karibu sana ndugu msomaji na mfuatiliaji wa mtandao wa isaackzake. Pia nikukaribishe katika ukurasa huu maalum kabisa kwa lengo la kufuatilia mambo mbalimbali tunayotarajia kujifunza kwa lengo la kuboresha maisha yetu. Moja ya eneo ambalo linaathiri maisha yetu kwa sehemu kubwa ni aina au mfumo wa elimu ambao tumepitia. Mfumo huo unaweza kuwa rasmi au usio rasmi, kwa vyovyote vile aina ya elimu ina sehemu kubwa sana katika kuamua hatma ya maisha yetu. Katika makala iliyopita tulijifunza juu ya ‘Asili au Historia ya mfumo rasmi wa elimu’. Leo tunajifunza juu ya changamoto za mfumo rasmi wa elimu. Karibu sana.
Asili ya Mfumo wa Elimu
Katika makala iliyopita tumeweza kuona juu ya asili ya mfumo rasmi wa elimu. Tumejifunza juu ya uanzishwaji wake na kusudi la kueneza mfumo husika. Tumeona hitaji kubwa la wamiliki wa viwanda kupata rasilimali watu kwa ajili ya kuzalisha. Huu ndio mfumo ulioletwa pia katika nchi za Afrika.
Hatahivyo, dunia imekumbwa na mabadiliko makubwa sana toka mfumo huu rasmi uanze kutumiwa karne ya 17 mpaka sasa karne ya 21. Maendeleo ya sayansi na teknolojia yanaufanya mfumo huu kuonekana na changamoto nyingi za kushindwa kukidhi mahitaji ya kizazi cha wasomi wa sasa.
Karibu katika kila sekta za uzalishaji, mifumo imebadilika, lakini katika eneo la kuzalisha rasilimali watu yaani sekta ya elimu, hakuna mabadiliko mengi. Huu ndio msingi wa kujikuta mataifa yanazalisha wasomi wengi wa darasani lakini hawana uwezo wa kuajirika au kujiajiri au kuanzisha miradi ya kutengeneza ajira kwa wengine.
Changamoto za Mfumo rasmi wa elimu
Kama nilivyoeleza katika utangulizi wa makala hii juu ya sekta ya elimu kutokuwa na mabadiliko makubwa ni kiini cha changamoto zinazoikumba sekta hiyo hasa katika nchi zinazoendelea. Katika mfululizo wa makala hizi tutaangalia changamoto zinazoikabili sekta ya elimu na namna inavyoathiri uwezo wa wanafunzi wa ngazi mbalimbali.
Kutokubadilika kwa mifumo ya elimu
Mifumo rasmi ya elimu imekuwepo kwa karne takribani 4 yaani kwa kipindi cha miaka 400. Ingawa mifumo hii ya elimu imechangia pakubwa maendeleo ya sayansi na teknolojia lakini kwa sehemu kubwa mifumo ya utoaji wa elimu haijabadilika. Hiki ndicho kiini cha tatizo la nchi nyingi. Mahitaji ya wakazi wa dunia wa karne ya 17, 18, 19 na 20 ni tofauti sana na mahitaji ya wakazi wa dunia wa karne hii ya 21. Namna ya kufanya kazi kwa watu wa zamani ni tofauti sana na watu wa sasa. Hivyo hatupaswi kuwaandaa watoto au viongozi wa baadae kama mababu zetu walivyoandaliwa katika zama za utumwa.
Nchi za Afrika zinapaswa kukaa chini na kufanya tathmini juu ya aina za elimu zao, na kufanya mabadiliko yanayostahili, ili kukidhi mahitaji ya kidunia. Kila taifa lina nchango wake katika dunia na namna sahihi ya kupata maarifa na jinsi ya kutoa mchango wa taifa hilo kwa dunia. Tunapawa kujifunza kwa wengine kwa lengo la kutengeneza mifumo ambayo itatufaa sisi kukabiliana na changamoto zetu.
Endelea kufuatilia mfululizo wa makala hizi ili kuona namna changamoto za mfumo rasmi wa elimu zinavyoathiri ubora wa wanafunzi na uwezo wa kutenda kazi za kimaendeleo.
‘Mungu ibariki Afrika’
Isaack Zake
Wakili, Mwalimu na Mshauri
Isaack Zake ni wakili wa kujitegemea na mshauri katika masuala mbalimbali ya sheria za kazi na rasilimali watu, ndoa na sheria za ardhi na mikataba. Isaack Zake ni mwanzilishi wa mtandao wa kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria wa www.ulizasheria.co.tz ni mwandishi wa vitabu na makala mbalimbali kwenye nyanja za kisheria, kijamii, kiuchumi na kiroho na mwalimu wa makundi mbalimbali ya kijamii kupitia mtandao wa www.isaackzake.co.tz . Isaack Zake pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Sheria na Uhusiano wa chama cha Waajiri TAACIME – www.taacime.co.tz.
Wasiliana na Isaack Zake kwa barua pepe info@isaackzake.co.tz au kwa simu 0713 888 040 kwa ushauri na mafundisho.
Leave a Reply
Want to join the discussion?Feel free to contribute!