
Utangulizi
Karibu sana ndugu msomaji na mfuatiliaji wa mtandao wa isaackzake. Pia nikukaribishe katika ukurasa huu maalum kabisa kwa lengo la kufuatilia mambo mbalimbali tunayotarajia kujifunza kwa lengo la kuboresha maisha yetu. Moja ya eneo ambalo linaathiri maisha yetu kwa sehemu kubwa ni aina au mfumo wa elimu ambao tumepitia. Mfumo huo unaweza kuwa rasmi au usio rasmi, kwa vyovyote vile aina ya elimu ina sehemu kubwa sana katika kuamua hatma ya maisha yetu. Katika makala iliyopita tulijifunza zaidi juu ya ‘Kusudi la Elimu’. Leo tunajifunza juu ya ‘Asili au Historia ya mfumo rasmi wa elimu’. Karibu sana.
Mfumo wa Elimu wa Afrika
Mfumo huu wa elimu ambao tunaita mfumo rasmi, kwa nchi zetu za Kiafrika ni mfumo ulioletwa kwa njia ya ukoloni. Kabla ya kuwepo mfumo huu, Afrika ilikuwa na njia zake za asili za kuhamisha maarifa kutoka kwa kizazi kimoja kwenda kwa kizazi kingine. Kila jamii kulingana na ujuzi wa aina ya shughuli walizofanya waliweza kurithisha maarifa hayo kwa jamii husika. Mfano jamii za wakulima, au wafugaji au wavuvi au walindaji wote waliweza kurithisha maarifa hayo kwa vizazi vingine kupitia mafunzo kwa vitendo.
Hatahivyo, ujio wa wakoloni katika nchi za Afrika ulianzisha mfumo wa elimu mwengine wenye lengo la kukidhi mahitaji ya wakoloni kwa wakati huo. Hapo ndipo tukaanza kuletewa aina za elimu za kikoloni na mitaala ambayo tumeendelea kurithisha vizazi vyetu hata baada ya zaidi ya nusu karne tangu nchi za Afrika kujipatia uhuru.
Asili ya mfumo rasmi wa elimu
Swali muhimu ambalo tunapaswa kujiuliza sisi waafrika ni nini asili ya mfumo huu rasmi wa elimu tulioletewa? Ni kitu gani kilisababisha wakoloni kuanzisha mfumo rasmi wa elimu wa watoto au wanafunzi kuingia madarasani kufundishwa vitu sawasawa?
Nchi za wakoloni walikuwa na mifumo yao ya kielimu kabla ya mapinduzi ya viwanda katika karne ya 17. Waliokuwa na uwezo wa kifedha waliweza kuwapatia watoto wao elimu kupitia waalimu maalum katika maeneo maalum ya kimaarifa. Hatahivyo, mabadiliko makubwa ya kisera na kisheria kuhusu elimu yalitokea mnano karne ya 17 ambapo suala la elimu lilifanyika kuwa lazima kwa watu wote hasa kwa wale waliokuwa wakifanya kazi katika viwanda. Hivyo mapinduzi ya viwanda na ongezeko la uhitaji wa rasilimali watu vilisababisha kuanzishwa mfumo rasmi wa elimu ili kukidhi mahitaji ya viwanda katika uzalishaji wa bidhaa.
Msingi mkubwa katika kutoa elimu kwa wafanyakazi wa viwanda ni kuwawezesha katika kufahamu maeneo makuu matatu yaani Kusoma, Kuandika na Kuhesabu au ‘KKK’. Haya ndio mambo ya msingi yaliyosisitizwa katika elimu, na ndio tunaendelea kusisitiza hata sasa katika elimu zetu.
Aina ya mfumo huu wa elimu ndio nchi zetu za Afrika tuliletewa na tukaurithi kuendelea katika maisha ya vizazi vyetu.
Endelea kufuatilia mfululizo wa makala hizi ili kuona jinsi aina ya mfumo rasmi wa elimu ulivyoathiri mifumo ya asili ya Afrika katika kujifunza.
‘Mungu ibariki Afrika’
Isaack Zake
Wakili, Mwalimu na Mshauri
Isaack Zake ni wakili wa kujitegemea na mshauri katika masuala mbalimbali ya sheria za kazi na rasilimali watu, ndoa na sheria za ardhi na mikataba. Isaack Zake ni mwanzilishi wa mtandao wa kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria wa www.ulizasheria.co.tz ni mwandishi wa vitabu na makala mbalimbali kwenye nyanja za kisheria, kijamii, kiuchumi na kiroho na mwalimu wa makundi mbalimbali ya kijamii kupitia mtandao wa www.isaackzake.co.tz . Isaack Zake pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Sheria na Uhusiano wa chama cha Waajiri TAACIME – www.taacime.co.tz.
Wasiliana na Isaack Zake kwa barua pepe info@isaackzake.co.tz au kwa simu 0713 888 040 kwa ushauri na mafundisho.
Leave a Reply
Want to join the discussion?Feel free to contribute!