Utangulizi

Karibu sana ndugu msomaji wa makala mbalimbali katika mtandao huu wa isaackzake. Tunamshukuru Mungu sana kwa nafasi aliyotupa tena kukutana na wewe msomaji kwa njia ya makala hizi.
Katika makala iliyopita tulijifunza juu ya Mamlaka ya Juu kutambua juu ya siku zako zote. Leo tunazidi kuangalia juu ya ufahamu wa Mamlaka ya Juu kabla ya kuumbwa Ulimwengu. Karibu tujifunze.
Kila siku tunashuhudia watu wengi walio katika msongo wa mawazo kuhusiana na aina ya maisha waliyonayo. Maisha yanaonekana ni mtihani mgumu sana kwa wakaazi wa dunia katika nyakati hizi. Kila mmoja yupo bize kuhakikisha anafanikisha mahitaji yake na yale ya familia.
Hali hii inapelekea kutokuaminiana, kutokuheshimiana kwa watu wengi sana. Upendo wa wengi umeondoka na tunashuhudia ukatili wa kiwango kikubwa kila kukicha. Hofu inaendelea kuongezeka sana kila leo kutokana na mazingira yanavyobadilika. Tunasikia hofu za magonjwa makubwa ambayo yanaangamiza watu kila leo, hofu ya ajali, hofu za kufanyiwa ukatili nk
Lakini kwa jinsi sisi tusivyojua tumekuwa tukirudisha lawama kwa Mamlaka ya Juu ya kwamba hatujali wala kutuangalia changamoto zetu. Wengi wamevunjika mioyo na kudhani ya kuwa hakuna Mungu kwenye dunia ya leo.
Maandiko yanaeleza wazi juu ya Mamlaka ya Juu kutuchagua na kutuwekea mfumo wa maisha katika nyakati hizi kwa ajili ya makusudi yake. Tuone jinsi anavyoeleza;
‘Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, aliyetubariki kwa baraka zote za rohoni, katika ulimwengu wa roho, ndani yake Kristo; kama vile alivyotuchagua katika yeye kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu, ili tuwe watakatifu, watu wasio na hatia mbele zake katika pendo.’ Efe.1:3-4
Tunaona wazi ya kuwa Mungu kwa neema yake alituchagua kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu. Hii ina maana kabla Mamlaka ya Juu haijaumba dunia hii tunayoishi tayari tulishachaguliwa ndani yake kwa KUSUDI lake maalum. Hatujaja hapa kwa bahati mbaya wala hatupaswi kupoteza matumaini katika maisha yetu kutokana na kile kinachoendelea hapa duniani. Mamlaka ya Juu ilituchagua kwa lengo la kututenga kwa ajili ya kusudi lake na kutuondolea hatia mbele zake.
Maisha yetu hayawezi kuwa na maana kwetu kama hatutalijua KUSUDI la maisha yetu. Hofu, hatia, masumbufu ya maisha, na msongo wa mawazo hautaweza kuondoka ndani yetu kama hatutajua ni kwa nini mimi na wewe tupo hapa siku ya leo. Njia pekee ya kufanya maisha yetu yawe na maana kwetu, kwa jamii inayotuzunguka, kwa ufalme wa Mungu ni kutambua kusudi maalum ambalo tumeumbwa kulitimiza.
Nikutakie baraka za Muumba katika kufuatilia hatua mbalimbali za kukuwezesha kulitambua kusudi la maisha yako na kulifanyia kazi.
Isaack Zake
Wakili, Mwandishi na Mshauri
Isaack Zake ni wakili wa kujitegemea na mshauri katika masuala mbalimbali ya sheria za kazi na rasilimali watu, ndoa na sheria za ardhi na mikataba. Isaack Zake ni mwanzilishi wa mtandao wa kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria wa www.ulizasheria.co.tz ni mwandishi wa vitabu na makala mbalimbali kwenye nyanja za kisheria, kijamii, kiuchumi na kiroho na mwalimu wa makundi mbalimbali ya kijamii kupitia mtandao wa www.isaackzake.co.tz . Isaack Zake pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Sheria na Uhusiano wa chama cha Waajiri TAACIME – www.taacime.co.tz.
Wasiliana na Isaack Zake kwa barua pepe info@isaackzake.co.tz au kwa simu 0713 888 040 kwa ushauri na mafundisho. Mungu akubariki sana.
Leave a Reply
Want to join the discussion?Feel free to contribute!