Utangulizi
Karibu sana ndugu yangu msomaji ni siku nyingine tena tumepewa na Mungu kwa ajili ya kuendelea kujifunza zaidi misingi ya chakula cha kiroho ili kutuwezesha kufanya mapenzi yake na kumtumikia kwa furaha na upendo siku ya leo.
‘Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu’ Yn.6:53
Mambo ya kujifunza
- Bwana Yesu anaeleza wazi wazi kwa Wayahudi waliokuwa wakishindana kuhusiana na neno alilotamka kuhusiana na kuula mwili wake. Hapa anaeleza ya kuwa ili mtu awe na uzima ndani yake ni lazima ale mwili wake Yesu Kristo na kuinywa damu yake.
- Huu ndio msingi wa chakula cha kiroho kwamba kila siku tupate kulishwa neno lake Yesu Kristo ambalo ni mwili wake. Kama tunavyofahamu umuhimu wa chakula siku zote ni kutupatia nguvu za kutenda kazi na kutuwezesha kuishi.
- Bila chakula cha kimwili hatuwezi kutenda kazi zetu ipasavyo wala kuishi kwa muda tunaopaswa kuishi. Mtu akipoteza uwezo wa kula chakula katika mwili hupoteza uwezo pia wa kutenda kazi na hatimaye hupoteza maisha.
- Kupata uzima ndani yetu tunahitaji kula mwili wa Kristo na kuinywa damu yake ili kuwa hai katika utu wetu wa ndani. Uhusiano wetu na Mungu unategemea ni kwa kiwango gani tunamtegemea katika kutupatia chakula cha kiroho kila siku.
- Uzima wetu unategemea kiwango na kiasi tunachopokea kila siku kutoka kwa Yesu Kristo neno ambalo amelihuisha kwa ajili yetu. Hupaswi kujiuliza endapo uhusiano wako na Mungu upo hai au la kama huna mazoea au tabia ya kupokea chakula cha kiroho kutoka kwake.

- Tumia nafasi hii ya leo kujenga uhitaji ndani yako wa kulisikia neno la Kristo kwa ajili yako binafsi kwa sababu lipo tayari kwa ajili yako ili kuhuisha maisha yako siku ya leo. Uzima wako ni maamuzi binafsi kama vile uzima wangu ni maamuzi yangu binafsi, kama nikitaka kuishi katika uzima wa Kristo sina budi kupokea mwili wake kila siku.
MAOMBI LEO
Ndugu yangu ikiwa ndani yako unashuhudiwa bado huna uhakika wa maisha yako na kumjua Mungu ipasavyo, ujue unahitaji ufahamu huo kupitia uzima wa Mungu kuingia ndani yako. Karibu ufuatane nami katika kuomba maombi haya ili uzima wa Mungu ukae ndani yako sasa;
‘Ee Mungu Baba ninakushukuru kwa neno lako la uzima, asante kwa sadaka ya Mwana wako Yesu Kristo pale msalabani kwa ajili yangu. Bwana Yesu ninakiri udhaifu wangu na wasi wasi wangu wa kupotea milele endapo nitaondoka katika maisha haya. Ninaomba unisamehe dhambi zangu zote nilizofanya na hata kuondoa asili ya dhambi ndani yangu, unitakase kwa Damu yako takatifu. Ninaomba ufute jina langu katika kitabu cha hukumu na kuliandika katika kitabu cha uzima. Ninaomba uniokoe na kunifanya upya ndani yangu kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Uingie ndani yangu na kuniongoza tangu sasa na hata milele’ Amen.
Ikiwa umefanya sala hii kwa imani, Mungu kwa neema yake amekurehemu na kukusamehe kabisa, hata kama umefanya dhambi yeye ameisafisha na kuisahau. Unapaswa na wewe kujisamehe na kumfuata Yesu tangu sasa.
Mungu mwenyewe aliyetuita ni mwaminifu, naye atafanya katika Jina la Mwana wake Mpendwa Yesu Kristo, Bwana na Mwokozi wa maisha yetu. Amen
‘Utupe leo riziki yetu’
Isaack Zake
Wakili, Mwalimu na Mshauri
Wasiliana na Isaack Zake kwa barua pepe info@isaackzake.co.tz au kwa simu 0713 888 040 kwa ushauri na mafundisho. Mungu akubariki sana
Leave a Reply
Want to join the discussion?Feel free to contribute!